Habari Mpya

Friday, 1 September 2017

MAMBA Wawili waliokwishaua watu wawili pamoja na mifugo kadhaa, wakiwemo ng’ombe na mbuzi, wameuawa na wananchi wa kijiji cha Igundu wilayani Bunda, mkoa wa Mara, baada ya kutaka kukamata ng’ombe waliokwenda kunywa maji katika ziwa Victoria.


Kaimu afisa mtendaji wa kata ya Igundu, Tekele Muligawe juzi alithibitisha kutokea kwa tukio hilo, lililotokea hivi karibuni katika kisiwa cha Chugu kilichoko ndani ya ziwa Victoria wilayani Bunda.

Muligawe alisema kuwa mamba hao walikuwa ni kero kubwa kwa wakazi wa kata hiyo, pamoja na kata za jirani, wanaokwenda kufanya shughuli za kibinadamu katika ziwa hilo.

Alisema kuwa kwa kipindi kisichozidi miezi miwili mamba hao walikuwa wamekwishaua watu wawili na ng’ombe watatu na kujeruhi ng’ombe wengine kadhaa, huku baadhi ya watu wakinusurika kukamatwa na mamba hao.

Alisema kuwa matukio hayo yalitokea wakati huu wa kiangazi na kwamba tayari taarifa hiyo alikwishaiwasilisha katika ngazi ya Wilaya hiyo.

“Kwa kipindi cha miezi isiyozidi miwili tayari hao mamba wameshakamata na kuua watu wawili na ng’ombe watatu. Kwa ujumla wake walikuwa ni kero, kubwa kwa wananchi wa maeneo hayo” alisema.

Alisema kuwa siku ya tukio mamba hao walitaka kukamata ng’ombe waliokuwa wamekwenda kunywa maji katika ziwa Victoria, hali iliyosababisha wananchi kuanza msako na kufanikiwa kuwaua.


Alisema kuwa baada ya kufanikiwa kuwaua walitoa nyongo zao na kuzitupa ndani ya shimo lefu la choo kwa ajili ya usalama wa watu kwani hiyo ni sumu kali.

Leave a Reply

Subscribe to Posts | Subscribe to Comments

- Copyright © Mito Ya Baraka Morogoro - Mito Ya Baraka Morogoro - Powered by Blogger - Designed by Peter Mwamkamba -