Habari Mpya

Monday, 21 August 2017

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imewaasa wakulima wa korosho nchini kuongeza uzalishaji wa korosho ili kuchangamkia fursa za masoko ya zao hilo linalohitajika zaidi katika masoko ya Marekani, Vietnam na India.
 
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo Francis Assenga 
Wito huo umetolewa jana na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Francis Assenga wakati akifungua Warsha ya Siku ya Wadau wa Vyama vya Ushirika inayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara.

Assenga alisema kuwa mahitaji ya korosho ni makubwa sana katika soko la dunia hivyo wakulima wa zao hilo hawana budi kujizatiti ili kuhakikisha wanazalisha kiasi kikubwa cha korosho ili kufikia au kuzidi malengo ya mavuno kwa msimu ujao ambayo yanakadiriwa kufikia kati ya tani laki tatu (3) hadi laki nne (4) ukilinganisha na takribani tani laki mbili na nusu kwa msimu uliopita.

Assenga alisema kuwa korosho ni zao la kimkakati ambalo likiwekezwa kwa usahihi linaweza kunyanyua uchumi na kipato kwa wakulima wa mikoa ya kusini na pwani ambao niyo ni wazalishaji wakuu wa zao hilo.

“Nawaasa mujitahidi kulima kisasa ili kuweza kufikia au kuvuka malengo ya mavuno ya msimu huu hali itakayowaongezea kipato hivyo kufikia malengo ya serikali ya kuwanyanyua wakulima nchini,” alisema.

Kaimu Mkurugenzi huyo wa TADB aliongeza kuwa Benki yake imejipanga kusaidia mfumo wa Stakabadhi ya maghala ili kuhakikisha kuwa malengo ya mavuno ya korosho kwa msimu huu yanafikiwa.

“TADB iko tayari kuratibu mfumo wa malipo ya fedha zitokanazo na mauzo ya korosho kwa njia ya TEHAMA, pia kwa kushiriakiana na soko la mazao (TMX), kusimamia ununuzi wa mazao kwa njia ya mtandao (electronic auction),” aliongeza

Aliongeza kuwa Benki ipo tayari kusimamia uuzaji wa mazao kwa mifumo ya salama ya kimataifa ya malipo kama vile dhamana ya malipo.
Naye Mkurugenzi wa Biashara wa Mikopo wa TADB, Bw. Augustino Chacha alisema kuwa Benki ya Kilimo ipo tayari kutoa mikopo kwa ajili ya uendelezaji wa miundombinu ya umwagiliaji na maghala na uzalishaji wa mbegu bora za mazao ya korosho na mihogo.

Aliongeza kuwa TADB pia ipo tayari kuviwezesha  viwanda vya kubangua mazao ya korosho, na kusindika ufuta, mihogo pamoja na uanzishaji wa mashamba mapya na ya kisasa ya korosho na ufuta.

“Tupo tayari kutoa mikopo kwa ajili ya kuwanyanyua wakulima kama ilivyolengwa na Serikali kupitia mikopo ya pembejeo kuongeza tija kwenye uzalishaji, miundo mbinu ya umwagiliaji na ununuzi wa zana za kilimo (kama matrekta, pump),” alisema.

Chacha aliongeza kuwa kwa kutambua umuhimu wa uhifadhi wa mazao ya kilimo, Benki ya Kilimo ipo tayari kutoa mikopo kwa ajili ya kujenga maghala mapya au kuboresha yaliyopo pamoja na kununua mizani ya kisasa na ununuzi wa magari ya usafirishaji mazao.

Akizungumzia nafasi ya taasisi za kifedha katika kudhibiti upotevu wa mapato kwa wakulima, Mkuu wa Kilimo na Fedha Vijijini wa Mfuko wa Kukuza Sekta ya Fedha (FSDT), Bw. Mwombeki Baregu alisema taasisi na mitandao ya simu nchini zina wajibu wa kubuni teknolojia rafiki wa wakulima itakayosaidia kudhibiti utapeli na wizi wa fedha za wakulima.

Baregu alisema teknolojia duni na ukosefu wa elimu sahihi juu ya matumizi na uhifadhi wa fedha umepelekea wakulima wengi nchini kupoteza mapato yao kwa kushindwa kufahamu uwekezaji sahihi wa fedha hizo.


“Naziomba taasisi za kifedha na mitandao ya simu za mkononi kuwasaidia wakulima katika kuhifadhi fedha zao ili kujiwekea akiba itakayowasaidia wakati wa maandalizi ya kilimo kwa msimu ujao na shughuli nyingine za kimaendeleo,” alisema.

Leave a Reply

Subscribe to Posts | Subscribe to Comments

- Copyright © Mito Ya Baraka Morogoro - Mito Ya Baraka Morogoro - Powered by Blogger - Designed by Peter Mwamkamba -